KARIAKOO KUENDELEA KUWEKA MAZINGIRA WEZESHI KWA WANAWAKE
Shirika la Masoko ya Kariakoo litaendelea kuweka mazingira rafiki kwa wanawake wanaofanya biashara katika soko la Kariakoo ikiwemo wafanya biashara wadogo ili kuhakikisha wanajikwamua kiuchumi na hivyo kukuza kipato cha familia na jamii kwa ujumla.
Kauli hiyo imetolewa na Meneja Mkuu wa shirika hilo, CPA. Ashraph Abdulkarim alipokuwa akieleza jitihada za Shirika la Masoko ya Kariakoo ilizofanya katika kumkomboa mwanamke na kukuza kipato chake na kuondokana na umasikini.
Amebainisha kuwa kwa kuwawekea wanawake mazingira wezeshi ya biashara watachangia pato la taifa kama ilivyoelekezwa katika Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050 ambayo inatambua mchango wa makundi mbalimbali katika kukuza uchumi wa nchi.
CPA. Abdulkarim ameongeza kuwa katika mpango mkakati wa shirika hilo wa miaka mitano kuanzia mwaka 2026-2031 umezingatia makundi yote ya jamii ikiwemo wanawake wanaofanya biashara wakubwa, wakati na wadogo.
CPA. Abdulkarim amesema katika mikakati ya kuboresha mazingira kwa wanawake ni pamoja na kutenga eneo maalum kwa ajili ya wakina mama kuwanyonyesha watoto wao, miundombinu kwa ajili ya watu wenye ulemavu na kwasasa shirika lipo kwenye hatua za awali za kuanzisha kituo cha kulea watoto ikiwa ni utekelezaji wa maagizo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alipokuwa akifungua soko la Kariakoo Februari 8, 2026.
Aidha, Shirika kwa kushirikiana na taasisi za kifedha zimeendelea kutoa elimu ya fedha kwa wafanyabiashara wakiwemo wanawake kuhusu uwekezaji, kujiwekea akiba, kukuza kipato na namna wanayoweza kufanya kupata ili kupata mikopo kutoka taasisi hizo.
Copyright ©2024 Shirika la Masoko ya Kariakoo . All rights reserved.