Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Prof. Mohamed Janabi, amewataka watumishi wa Shirika la Masoko ya Kariakoo kujenga utamaduni wa kupima afya angalau mara moja kwa mwaka.
Alisema hatua hiyo itasaidia kutambua mapema dalili za magonjwa sugu yasiyoambukiza na hivyo kupata tiba kwa wakati, kuepusha athari zinazoweza kupunguza nguvu kazi ya taifa.
Prof. Janabi alitoa ushauri huo alipokuwa akizungumza wakati wa mafunzo ya siku moja kwa watumishi wa shirika hilo yaliyofanyika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili ( Mei 9, 2025).
Katika mada yake kuhusu ugonjwa wa kiarusi, alieleza kuwa mtindo mbaya wa maisha, shinikizo la juu la damu, unywaji pombe kupita kiasi, na ulaji wa vyakula vyenye sukari na mafuta mengi ni sababu kuu zinazochangia ugonjwa huo.
"Ni muhimu kufanya uchunguzi wa afya zenu kila mwaka ili kuepuka kugundua magonjwa mkiwa katika hatua za mwisho au uzeeni, hali ambayo inaweza kusababisha madhara makubwa kwa afya zenu," alisisitiza Prof. Janabi ambaye ni mtaalamu bingwa wa magonjwa ya moyo.
Prof.Janabi aliongeza kuwa dunia inakabiliwa na magonjwa mengi hatari kama vile moyo, shinikizo la damu, kisukari, figo, na kiarusi, ambayo yanasababisha vifo vingi. Hivyo, upimaji wa afya wa mapema ni muhimu ili kujua dalili na kupata matibabu stahiki.
Meneja Mkuu wa Shirika la Masoko ya Kariakoo, CPA. Ashraph Abdulkarim, alieleza kuwa shirika limeandaa mafunzo hayo kama sehemu ya mkakati wa kuwajengea uwezo watumishi wake ili waweze kufahamu hali zao za afya na kuchukua hatua za mapema kudhibiti magonjwa.
CPA Abdulkarim alishukuru Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa kutoa mafunzo kwa watumishi 35 ambao wana jukumu muhimu la kuhudumia wafanyabiashara na wananchi katika soko hilo.
Katika mada nyingine, Dkt. Garvin Kweka aliwaasa watumishi kuwa waaminifu kwa wenzi wao na kuchukua tahadhari dhidi ya maambukizi ya VVU/UKIMWI kwa kuepuka ngono zembe na matumizi mabaya ya vileo.
Naye Afisa Mwelimishaji kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Ilala, Bi. Mary Mwakyusa, aliwaonya watumishi dhidi ya vitendo vya rushwa wanapohudumia wafanyabiashara wa Soko la Kariakoo.
General Manager, Kariakoo Markets Corporation, Nyamwezi/Tandamti Street,
Postal Address: P. O. Box 15789 Dar es Salaam, Tanzania
Telephone: +255 22 2180678
Mobile:
Email: info@kariakoomarket.co.tz
Copyright ©2024 Shirika la Masoko ya Kariakoo . All rights reserved.