ZAIDI YA WANANCHI 700 WATEMBELEA BANDA LA KARIAKOO NANENANE DODOMA
Zaidi ya wananchi 700 wa mkoa wa Dodoma na maeneo ya jirani wamepata huduma katika Banda la Shirika la Masoko ya Kariakoo ndani ya maonesho ya Kimataifa ya Kilimo Nanenane yanayofanyika kitaifa katika viwanja vya John Samwel Malecela, Nzuguni mkoani Dodoma.
Idadi hiyo inalifanya shirika hilo kuwa miongoni mwa taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI kuhudumia watu wengi zaidi na hivyo kuonesha ni kwa kiasi gani wananchi wanahitaji kupata taarifa za shirika hilo ambalo linamiliki Soko la Kuu la Kariakoo, soko ambalo mapngilio wake wa biashara umezingatia makundi mbalimbali ya jamii.
Miongoni mwa mapendekezo yaliyotolewa na wananchi waliotembelea banda la shirika hilo ni uongozi wa Shirika la Masoko ya Kariakoo kuanzisha masoko mengine ndani na nje ya Dar es Salaam yenye hadhi na bidhaa kama zinazopatika na Kariakoo ili kupunguza usumbufu wa kuzifuata huduma hizo Dar es Salaam au mitaa ya Kariakoo.
Akizungumza katika banda hilo, Meneja Mkuu wa Shirika hilo CPA. Ashraph Abdulkarim amesema kwa kutambua umuhimu wa Maonesho ya Kimataifa ya Kilimo (Nanenane), shirika limeamua kusogeza huduma karibu na wakulima kwakuwa kwa kiasi kikubwa biashara inayofanyika Soko Kuu la Kariakoo zinagusa wakulima na wafugaji katika maeneo ya pembejeo, biashara ya nafaka nk.
CPA. Abdulkarim amebainisha kuwa maonesho hayo yameimarisha mahusiano na wadau mbalimbali ambao wameona fursa ya kushirikiana na Soko hilo katika nyaja mbalimbali kwa lengo la kuongeza tija baina ya taasisi hizo.
Maonesho ya Kimataifa ya Nanenane kitaifa yamefungwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan Agosti 8, 2025.
Copyright ©2024 Shirika la Masoko ya Kariakoo . All rights reserved.